KIPINDUPINDU,UAMBUKIZWAJI,DALILI,KUJIKINGA,NA MTIBABU

By
Advertisement

Ugonjwa Wa Kipindupindu

   
Kipindupindu ni ugonjwa wa kuambukiza wa kuharisha unaosababishwa na vijidudu vya bakteria. Ugonjwa huu hutokana na matumizi ya maji yasiyo safi au chakula kilichoandaliwa katika mazingira yasiyo safi. Ugonjwa huu ni wa ghafla na kwa watu wengu hauleti dalili kali sana. Ingawa unatibika, kipindupindu kinaweza kuwa hatari sana na kuhatarisha maisha ya mgonjwa.

Maambukizi Ya Kipindupindu


Kipindupindu hutokana na maambukizi ya vijidudu vya bakteria viitwavyo Vibrio cholera. Vijidudu hivi hukaa kwenye majimaji, na wadudu kama nzi wanaweza kuvihamisha kutoka sehemu moja mpaka nyingine.
Maambukizi hutokea pale ambapo usafi wa maji, chakula, mazingira na binafsi haujazingatiwa. Kwa njia ya chakula vijidudu huingia kwenye utumbo na kisha kushambulia seli za utumbo. Dalili huanza kujionesha masaa 24 mpaka 48 baada ya maambukizi kutokea.

Dalili Za KIpindupindu


Kipindupindu huanza dalili masaa 24 mpaka 48 baada ya maambukizi. Huanza ghafla kwa kuharisha sana bila maumivu yoyote ya tumbo. Mwanzoni choo kinaweza kuwa kizito kidogo lakini baade kuwa chepesi kama maji, muonekano wako hufanana na maji ya mchele (maji baada ya kuosha mchele). Mgonjwa anaweza kuharisha mara nyingi sana kiasi cha kupata choo kwa mfululizo.
Baadae anaweza akaanza kutapika, akapata maumivu ya tumbo,kulegea na mwili kukosa nguvu kutokana na kupoteza maji na madini mengi sana.
Mara nyingi kipindupindu hakiambatani na homa. Wagonjwa wengi hupata dalili ambazo sio kali sana na kupona baada ya matibabu, wengine hupata dalili kali ambazo huchangia upungufu wa maji na mgonjwa kufariki.

Matibabu Ya Kipindupindu


Endapo unahisi una kipindupindu au kuna mtu ana kipindupindu basi wahi au mwahishe hospitali haraka!. Matibabu ya haraka ni muhimu kwa mtu mwenye ugonjwa wa kipindupindu. Kwa kiasi kikubwa ugonjwa hutambulika kwa dalili zake na uchunguzi wa daktari kwa mgonjwa. Pale unapojulikana matibabu ni muhimu ili kuzuia madhara yake. Kwa sababu ugonjwa huu huambukizwa kirahisi kwa njia ya maji na chakula, wagonjwa hutibiwa kwa kuwekwa sehemu za peke yao ili wasiambukize wengine.
Kumuongezea maji ni sehemu  muhimu ya matibabu kutokana na kupoteza maji mengi kwa kuharisha. Maji hupewa kwa njia ya mdomo kama ORS na kwa maji ya dripu.
Dawa kama Tetracycline, Ciprofloxacin na Doxycycline hutumika kwenye kutibu kipindupindu. Hizi zinasaidia kuua vijidudu vya kipindupindu ndani ya mwili.

Kujikinga na Kipindupindu


Usafi binafsi, chakula na mazingira ni muhimu ili kujikinga na kuzuia ugonjwa huu. Husambazwa kwa kutozingatia usafi na hivyo maji au chakula kuingiliwa na vijidudu vya ugonjwa huu. Ili kujikinga na kuzuia ugonjwa huu zingatia yafuatayo;
  • Nawa mikono yako kwa maji safi na sabuni kila baada ya kwenda chooni
  • Nawa mikono kwa maji safi kabla na baada ya kula chakula au matunda.
  • Osha matunda kwa maji safi kabla ya kula
  • Tumia maji ya kunywa safi yaliyochemshwa au kutakaswa kwa dawa na kuhifadhiwa katika chombo kisafi.
  • Hakikisha unakula chakula ambacho hakijapoa. Kiwe cha moto na kimehifadhiwa katika chombo kisafi.
  • Tunza mazingira yako yawe katika hali ya usafi. Usiruhusu nzi kuruka ruka au kutua kwenye chakula chako.
DUMISHA USAFI WAKO WA NDANI NA MAZINGIRA YAKO PIA NA WEWE MWENYEWE BINAFSI..
POLE KWA TATIZO HILI LINALOKUSUMBUA NAAMIN UTAPONA KWANI KUUMWA SIO KUFA BALI KUTHIBITISHA KAMA KWELI WEWE UNA AFYA NZURI NA MWILI WAKO UMEWEZA KUTOA MAGONJWA YALIYOTAKA KUKUSHAMBULIA KATIKA MWILI WAKO...

0 comments:

Mr.Kikoti. Powered by Blogger.

Comments